
Afisa Mwandamizi wa manunuzi Bodi ya michezo ya kubahatisha, Sadick Kasuhya kulia akimkabidhi mmoja ya madawati 100 yaliyotolewa kwa ufadhili wa Bodi ya michezo ya kubahatisha kwa Mbunge wa Viti maalum kupitia Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Iringa Lita Kabati tukio lililofanyika katika shule ya msingi Sabasaba mkoani Iringa.
====== ===== ======
Na Denis Mlowe,Iringa .
MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa(CCM) Lita Kabati ametoa msaada wa madawati 100 yenye thamani ya shilingi milioni 6.3 kwa shule za msingi zilizoko mkoani hapa.
Kabati akizungumza wakati akikabidhiwa madawati hayo kwa ufadhili wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania mwishoni mwa wiki, alisema shule nyingi mkoani hapa zina upungufu mkubwa wa madawati hivyo ni jukumu la kiongozi kuweza kusaidia kuondokana na hali hii na kuwashukuru bodi ya michezo ya kubahatisha Tanzania.
“Nimefanya ziara katika shule za msingi nyingi za mkoani kwangu kuna matatizo mengi kama ukosefu wa madawati na vitabu ndipo nikawaomba wenzetu wa bodi ya michezo kubahatisha wanisaidie madawati kwa shule hizi hakika ninawashukuru sana hakika haitamaliza tatizo lakini itasaidia kupunguza japo kwa uchache” alisema Kabati
Alisema kuwa elimu bora kwa wanafunzi wa shule za msingi unaendana na vifaa wanavyotumia katika kupata elimu ya msingi ikiwemo kakaa katika madawati bora kunachangia maendeleo ya taifa letu katika kukuza elimu.
Kabati aliwataka viongozi wengine kuondokana na tabia ya kufikiria kuwa katika kuleta maendeleo ya mkoa ni mojawapo ya kampeni bali ni kuungana na kuweza kupambana katika kuwaletea maendeleo wananchi wanaowawakilisha.
Akizungumza kabla ya kukabidhi madawati hayo kwa niaba ya mkurugenzi wa bodi ya michezo ya kubahatisha Tanzania, Afisa Mwandamizi wa manunuzi Bodi ya michezo ya kubahatisha, Sadick Kasuhya alisema moja ya majukumu ya bodi kuweza kusaidia jamii katika sekta ya elimu na wataendelea kusaidia shule mbalimbali nchini.
Alisema kuwa kwa msaada huu wa madawati 100 yenye thamani ya shilingi milioni 6, 3 kutasaidia kupunguza tatizo la madawati kwa baadhi ya shule zitakazokabidhiwa msaada huo.
0 comments:
Post a Comment