PADRI ALITISHIWA KIFO NA MTU ASIYEMJUA MIEZI MITATU ILIYOPITA - Sema Naye
Headlines News :
Home » » PADRI ALITISHIWA KIFO NA MTU ASIYEMJUA MIEZI MITATU ILIYOPITA

PADRI ALITISHIWA KIFO NA MTU ASIYEMJUA MIEZI MITATU ILIYOPITA

Written By Sema Naye - Naipenda Tanzania on Sunday, September 15, 2013 | 3:06 PM

Wananchi Z'bar walaumiwa kulea vitendo hivyo vya kikatili.

 
Septemba 15,2013- Jumapili.

DSM/ZANZIBAR: Baada ya siku moja kufanyika kitendo cha kikatili kwa Padri wa Kanisa Katoliki Parokia ya Cheju, Mkoa wa Kusini Unguja, Joseph Mwang’amba kumwagiwa tindikali na watu wasiojulikana, imebainika kuwa alitishiwa kuuawa miezi mitatu kabla ya kupatwa na tukio hilo.

Pindi Padri huyo akieleza yaliyomkuta, Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein, ameijia juu polisi kwa kushindwa kudhibiti matukio ya viongozi wa dini pamoja na kupewa taarifa za tahadhari na waathirika katika serikali visiwani humo, juu ya matukio tofauti ikiwa  ni pamoja na vitisho vya mauaji, pia kushambuliwa kwa kumwagiwa tindikali Dr Shein amelitaka jeshi la polisi kuwakamata waliohusika na tukio hilo.

Padri huyo, aliyejeruhiwa maeneo ya usoni, mikononi na kifuani baada ya kumwagiwa tindikali hiyo alisafirishwa jana na ndege ya kukodi ya Shirika la Coastal kutoka visiwani humo hadi Dar es Salaam na baadaye kupelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa matibabu zaidi.

Dk Shein alisema Polisi inatakiwa kuongeza nguvu za uchunguzi ili kukabiliana na matukio ya kikatili ya umwagaji wa tindikali, yanayoshamili visiwani humo hivi sasa.

“Hatuwezi kuviacha vitendo hivi viendelee … ni lazima Jeshi la Polisi lijitahidi kuwatafuta wahusika ili sheria ichukue mkondo wake,” alisema Dk Shein.

Dk Sheni alisema, kitendo hicho ni cha kikatili na kisichovumilika na kuongeza kuwa wahusika lazima wasakwe na kuchukuliwa hatua za kisheria.

Kwa upande wake, Padri wa Parokia ya Mtakatifu Joseph, Zanzibar, Thomas Assenga aliyefuatana na kiongozi huyo mpaka MNH, alisema siku za nyuma Padri Mwang’amba alitolewa vitisho na mtu ambaye hamfahamu wakati akienda kutoa huduma katika kituo cha wazee cha Welezo.

Alisema kabla ya kufika kituoni hapo, kuna eneo ambalo nyakati za asubuhi watu hufanya mazoezi barabarani ambapo kuna mtu mmoja alimtolea maneno ya vitisho.

“Unajua kawaida ya watu wa Zanzibar hufanya mazoezi barabarani, sasa kipindi anapita eneo hilo katika kilima, kuna mtu alimwambia atamfanyia kitu kibaya ambacho hatujui ndiyo hiki au la,” alisema Padri Assenga na kuongeza:

Alisema Juni mwaka huu mara baada ya kupewa vitisho hivyo alikwenda kutoa taarifa kwa Sheha wa eneo hilo na kituo cha polisi.

“Mara baada ya kutolewa vitisho hivyo Juni mwaka huu, alichukua jukumu la kwenda kutoa taarifa kwa mkuu wa eneo hilo (Sheha) na kituo cha polisi.”

Akielezea tukio la kumwagiwa tindikali Padri Mwang’amba, alisema alimwagiwa saa 9:45 alasiri juzi wakati akizungumza na simu nje ya internet café iliyopo eneo la Mlandege.

Padri Assenga alisema kabla ya kumwagiwa tindikali, Padri huyo alikuwa ndani ya internet akitoa ‘photocopy’ za nyaraka. Alipokuwa akitoa ‘photocopy’ (nakala) alipigiwa simu na mtu ambaye anamfahamu hivyo ikabidi atoke nje kuongea naye, lakini alivyokuwa akiongea alimwona kijana akija na kikopo alichokishika mkononi na kummwagia na kukimbia,”Padri Aseenga alisema.

Aliongeza kuwa mara baada ya tukio hilo, padre Joseph alipelekwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja, kwa matibabu baada ya kujeruhiwa usoni, kifuani na mikononi ambapo hivi sasa afya yake inaendelea vizuri.

Kwa upande wake Mohamed Muhina, Msemaji wa Jeshi la Polisi Zanzibar, alisema kuwa hajapata taarifa zozote za vitisho dhidi ya Padri hiyo badala yake ameahidi kulifanyia kazi tukio hilo na mengine kama hayo yaliyopita.

“Tukio limetokea mchana kweupe na watu walikuwapo lakini wananchi wamekuwa hawatupi ushirikiano hivyo tunawaomba kutupa ushirikiano ili kukomesha vitendo hivi,” alisema Muhina.

Tukio lilivyokuwa

Akifafanua zaidi kuhusu tukio hilo, Padri Mwang’amba alisema kwamba lilitokea nje ya duka linalotoa huduma za mawasiliano ya mtandao (Sun Shine Internet Caffee) liliopo eneo la Mlandege Wilaya ya Mjini Unguja, ndipo alipotokea kijana mmoja na kumwagia tindikali.

Padri Mwang’amba akimweleza Dk Shein kuwa hali yake si mbaya sana kwakuwa anaweza kuona vizuri, lakini anatarajia kupata nafuu zaidi baada ya uvimbe kupungua katika sehemu za usoni na machoni mwake.
“Hali yangu ni nzuri lakini natarajia uvimbe ukipungua nitaona vizuri zaidi,” alisema Padri Mwang’amba na kuongeza kuwa ilikuwa ni bahati kwake kwa kutoathirika sana.

Uwanja wa Ndege

Katika Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, Kiongozi huyo aliwasili saa 4.16 asubuhi na ndege ya Shirika la Costal akiongozana na Padri Assenge.

Padri huyo aliyeonekana kutembea taratibu, huku akijitahidi kujifunika mwili wake na kanga kuzuia mwanga wa Jua kutokuathiri zaidi mwili wake ulioathiriwa na tindikali.
Na Mwandishi wetu.
Share this article :

0 comments:

 
Support : 255-272-545-994 | Jasper A.K. | Mas Template
Copyright © 2011. Sema Naye - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger